Sura 4

1 Magombano na ugomvi vinavyokuwa kati yenu vinatoka wapi? Si vinatoka katika tamaa zenu zinazopigana ndani ya miili yenu? 2 Munatamani kupata kitu fulani, lakini hamukipati. Munaua na kusikia wivu, lakini hamuwezi kupata kitu. Na kwa hiyo, munagombana na kuwa na ugomvi. Hamupati kitu munachotaka kwa sababu hamukiombi kwa Mungu. 3 Wakati munapoomba, hamupati kitu kwa sababu munaomba kwa nia mbaya, kwa maana munataka vitu kusudi mutimize tu tamaa zenu. 4 Ninyi watu wasiokuwa na uaminifu! Hamujui kwamba kua rafiki wa dunia ni kuwa adui wa Mungu? Basi yeye anayetaka kupenda raha za dunia anajifanya mwenyewe kuwa adui wa Mungu. 5 Musizani kwamba ni kwa bure Maandiko Matakatifu yanasema: «Mungu anasikia wivu sana kwa ajili ya yule Roho aliyemuweka akae ndani yetu. 6 Lakini Mungu ametujalia neema kubwa zaidi, kwa maana Maandiko yanasema: “Mungu anapingana na wenye kiburi, lakini anawajalia wanyenyekevu neema.”» 7 Basi mumutii Mungu. Mupingane na Shetani, naye atawakimbia. 8 Mumukaribie Mungu, naye atawakaribia. Musafishe mikono yenu, ninyi wenye zambi! Mutakase mioyo yenu, ninyi wenye nia mbili! 9 Musikitike, mulie na kulalamika. Kucheka kwenu kugeuke kuwa kilio, na furaha yenu igeuke kuwa huzuni. 10 Mujinyenyekeze mbele ya Bwana, naye atawainua. 11 Wandugu, musisemeane ubaya. Yule anayesema ubaya juu ya ndugu yake au kumuhukumu, anasema ubaya juu ya Sheria na kuihukumu. Ukihukumu Sheria, wewe si mwenye kutii Sheria, lakini mwenye kuihukumu. 12 Mungu peke yake ndiye anayesimamisha Sheria na anayeweza kuhukumu. Ni yeye peke yake anayeweza kuokoa na kuangamiza. Basi wewe unayemuhukumu mwenzako, unajizania kuwa nani? 13 Munisikilize sasa, ninyi munaosema: «Leo au kesho tutakwenda katika mji fulani, tutakaa kule kwa muda wa mwaka mzima, tutafanya biashara na kupata faida. 14 Ninyi hamujui namna gani maisha yenu yatakavyokuwa kesho! Kwa maana ninyi ni kama muvuke unaoonekana kwa wakati kidogo, kisha unatoweka. 15 Ninyi mungepaswa kusema: “Kama Bwana anataka, tutaishi na kufanya hivi na hivi.”» 16 Lakini sasa munajivuna na kujisifu. Majivuno yote ya namna hii ni mabaya. 17 Basi, mtu anayejua kutenda mema wala hayatendi, anafanya zambi.