Sura 3

1 Wandugu zangu, kati yenu kusikuwe walimu wengi, kwa maana munajua vema ya kuwa sisi walimu tutahukumiwa vikali zaidi kuliko watu wengine. 2 Sisi wote tunakosa kwa njia mbalimbali. Mtu asiyekosa katika masemi yake, huyo ni mtu mukamilifu, naye yuko na uwezo wa kutawala mwili wake wote. 3 Tunaweka lijamu katika vinywa vya farasi kusudi watutii, na hivi tunaweza kuwaongoza miili yao kwenda fasi yote tunayotaka. 4 Muangalie vilevile mashua. Hata mashua ni kubwa sana na zenye kusukumwa na upepo mukali, zinaongozwa na usukani mudogo sana na kuendeshwa pahali kapiteni anapotaka. 5 Hivi vilevile ulimi ni kiungo kidogo cha mwili, lakini unaweza kujivunia mambo makubwa sana. Muangalie, moto kidogo inaweza kuchoma pori kubwa sana! 6 Nao ulimi ni kama moto. Ni dunia ya ubaya, ulimi ni kiungo kinachojaa ubaya wa kila namna. Ulimi unapatikana kwenye nafasi yake katikati ya viungo vyetu, nao ndio unaochafua mwili wote. Unateketeza maisha yetu ukichomwa wenyewe na moto unaotoka katika jehenamu. 7 Kila namna ya nyama, ndege, nyoka na samaki wanaweza kufugwa na mtu, na wamekwisha kufugwa naye. 8 Lakini hakuna mtu mmoja anayeweza kufuga ulimi, maana ni uovu usiotulia, unajaa sumu yenye kuua. 9 Kwa njia ya ulimi tunamusifu Bwana anayekuwa Baba yetu, na kwa njia ile ile tunalaani watu walioumbwa kwa mufano wa Mungu. 10 Ndani ya kinywa kimoja munatoka maneno ya sifa na ya laana. Wandugu zangu, mambo haya hayapaswi kuwa vile. 11 Maji matamu na maji machungu hayawezi kutiririka tokea fasi moja ndani ya kisima kimoja. 12 Wandugu zangu, muti unaotoa matunda ya tini unaweza kutoa matunda ya muzeituni? Au muzabibu unaweza kutoa matunda ya tini? Hapana! Hivi vilevile kisima kinachotoa maji ya chumvi hakiwezi kutoa maji matamu. 13 Nani anayekuwa na hekima na ufahamu kati yenu? Basi aonyeshe jambo lile kwa njia ya mwenendo wake mzuri, kwa njia ya matendo yanayofanyika katika upole unaotokana na hekima ile. 14 Lakini mukiwa na wivu wenye kuchangana na uchungu katika mioyo yenu pamoja na roho ya ugomvi, musijivune wala musigeuze maneno ya kweli kuwa uongo. 15 Hekima ya namna hii haitoki mbinguni; lakini ni ya dunia, nayo ni ya kimwili na ya kishetani. 16 Kwa maana pahali kunapokuwa wivu na roho ya ugomvi, kuko machafuko vilevile na kila tendo baya. 17 Lakini hekima inayotoka mbinguni, kwanza ni safi, tena ni yenye amani, upole na usikilivu, inajaa huruma na matendo mema. Haina upendeleo wala udanganyifu. 18 Na tunda la haki linapandwa katika amani na wale wanaopenda amani.