Sura 4

1 Kwa wema wake, Mungu ametupatia utumishi huu, na kwa sababu hii sisi hatukati tumaini. 2 Tumekataa mambo ya kisirisiri na ya haya. Hatuna mwenendo wa udanganyifu wala hatupotowi neno la Mungu. Lakini tunajulisha waziwazi ukweli kusudi tuvute kila mtu kutuaminia katika zamiri yake mbele ya Mungu. 3 Lakini kama Habari Njema tunayotangaza ni ngumu kwa kusikia, ni kwa wale tu wanaofuata njia ya upotevu. 4 Wao hawaamini kwa sababu yule mungu wa dunia hii amefunika akili zao. Yeye anawazuiza wasione mwangaza unaoletwa na Habari Njema ya utukufu wa Kristo, anayefanana na Mungu. 5 Kwa maana, hatutangazi habari zetu sisi wenyewe, lakini tunatangaza kwamba Yesu Kristo ndiye Bwana, nasi tuko watumishi wenu kwa ajili ya Yesu. 6 Yule Mungu aliyesema: «Mwangaza uangaze katika giza,» ndiye aliyeangaza ndani ya mioyo yetu, na kutuwezesha kufahamu utukufu wa Mungu unaongaa kwenye uso wa Kristo. 7 Lakini sisi tunaokuwa na hazina hii ya kiroho, tuko vyombo vya udongo, kusudi watu waone waziwazi uwezo huu wa ajabu sana unaotoka kwa Mungu lakini si kwetu sisi wenyewe. 8 Sisi tunagandamizwa kila namna, lakini hatushindwi; tunahangaishwa, lakini hatukati tumaini; 9 tunateswa, lakini Mungu hatuachilii; tunatupwa chini, lakini hatuangamizwi. 10 Kila wakati tunabeba mateso ya kufa kwa Yesu katika mwili wetu, kusudi uzima wa Yesu uonekane vilevile ndani ya mwili wetu. 11 Kwa maana katika maisha yetu, tunakuwa kila mara katika hatari ya kufa kwa ajili ya Yesu, kusudi uzima wake uonekane vilevile katika mwili wetu unaokuwa wa kufa. 12 Kwa hivi, kifo kinafanya kazi ndani yetu, lakini uzima unafanya kazi ndani yenu. 13 Maandiko Matakatifu yanasema: «Niliamini ndiyo maana nilisema.» Sisi vilevile kwa moyo tunakuwa na imani ile ile, ndiyo maana tunasema. 14 Tunajua kwamba Mungu aliyemufufua Bwana Yesu atatufufua sisi vilevile pamoja na Yesu. Yeye atatufikisha pamoja nanyi mbele ya Yesu. 15 Kwa maana mambo haya yote yanafika kwa ajili yenu kusudi neema ya Mungu izidishwe kwa watu wengi siku zote, nao wapate kumutolea Mungu shukrani nyingi kwa ajili ya utukufu wake. 16 Kwa sababu hii hatukati tumaini hata kidogo. Ijapokuwa hali yetu ya kimwili inaharibika, hali yetu ya kiroho inafanywa upya siku kwa siku. 17 Kwa maana taabu tunayopata ni ndogo na ya muda tu, inatutayarishia utukufu mkubwa sana na wa milele unaokuwa mzuri zaidi kupita mateso haya. 18 Maana sisi hatuangalii vitu vile vinavyoonekana, lakini vitu visivyoonekana. Kwa sababu vile vinavyoonekana vinadumu muda kidogo tu, lakini vile visivyoonekana, vinadumu milele.