Sura 5

1 Kwa maana, tunajua kwamba hema hii tunayoishi ndani yake hapa katika dunia, maana yake mwili wetu, itakapobomolewa, Mungu atatupatia makao mengine mbinguni. Nayo ni nyumba aliyoijenga yeye mwenyewe na inayodumu milele. 2 Na sasa katika hali hii tunaugua kwa maana tunatamani sana kuvaa makao yetu yanayotoka mbinguni. 3 Kwa maana, tukisha kuyavaa hatutaonekana tena kuwa uchi. 4 Hakika kwa wakati wowote tungali tunaishi katika makao haya ya dunia, tunaugua kwa kulemewa. Si kwa sababu tunataka kuondolewa mwili wa dunia, lakini tunataka kuvaa mwili wa mbinguni, kusudi uzima wa milele upate kubadilisha miili yetu inayokuwa ya kufa. 5 Ni Mungu mwenyewe aliyetuwezesha kupata mabadiliko hayo na kuweka Roho Mtakatifu ndani yetu kuwa rehani ya vitu vyote anavyotuwekea. 6 Basi tuna uhodari siku zote. Tunajua kwamba wakati tunapoishi katika mwili huu, tunaishi mbali na makao ya Bwana. 7 Kwa maana tunaishi kwa imani lakini si kwa kuona. 8 Sisi tuna uhodari na tungependa zaidi kutoka katika mwili huu na kwenda kuishi pamoja na Bwana. 9 Lakini mbele ya yote tunataka sana kumupendeza Bwana, ikiwa tunakaa au kutoka katika mwili huu. 10 Kwa maana sisi wote tunapaswa kusimama kwa kusambishwa mbele ya tribinali ya Kristo, kusudi kila mtu alipwe kufuatana na matendo yake mema au mabaya aliyofanya alipokuwa akiishi ndani ya mwili wake. 11 Basi, kwa sababu tunajua kwamba ni lazima kumwogopa Bwana, ndiyo maana tunajitoa kuwavuta watu kwake. Mungu anatujua waziwazi nami ninatumaini kwamba ninyi wenyewe munatujua waziwazi vilevile. 12 Sisi hatuanzi tena kujisifu wenyewe mbele yenu, lakini tunawapa ninyi sababu ya kuweza kujivuna kwa ajili yetu. Hivi tena munaweza kupata maneno ya kuwajibu wale wanaojivunia tu hali yao ya inje, lakini si mambo yanayokuwa ndani ya mioyo yao. 13 Ikiwa kweli tunaonekana kuwa wenda-wazimu, ni kwa ajili ya Mungu, lakini kama sisi ni wenye akili sawa, ni kwa faida yenu. 14 Maana upendo wa Kristo unatuongoza sisi tunaokubali kwamba ni mtu mmoja tu ndiye aliyekufa kwa ajili ya watu wote; maana yake wote wanashiriki katika kifo chake. 15 Naye alikufa kwa ajili ya watu wote, kusudi wale wanaoishi, wasiishi kwa ajili yao wenyewe, lakini kwa ajili ya yule aliyekufa na kufufuka kwa ajili yao. 16 Kwa hiyo basi, tangu sasa hatumuhesabu tena mtu yeyote kufuatana na hali ya kimtu. Hata ikiwa tulimuhesabu Kristo kufuatana na hali ya kimtu, kwa sasa hatumuhesabu tena kufuatana na hali ile. 17 Basi mtu yeyote anapoungana na Kristo, yeye anakuwa kiumbe kipya. Mambo ya zamani yametoweka, na sasa hali mupya imefika. 18 Mambo haya yote yalifanyika na Mungu, aliyetupatanisha naye kwa njia ya Kristo na kutupatia kazi ya kuongoza watu wengine wapatane naye. 19 Ndiyo kusema, Mungu ndiye aliyekuwa akipatanisha watu wote na yeye mwenyewe kwa njia ya Kristo bila kuhesabu makosa yao. Yeye ametupatia ujumbe wa upatanisho. 20 Basi sisi ni wajumbe wa Kristo. Kwa njia yetu, Mungu mwenyewe anawaita ninyi; na kwa hiyo tunawasihi katika jina la Kristo, mukubali kupatanishwa na Mungu. 21 Kwa maana Kristo alikuwa bila zambi, lakini Mungu alimubebesha muzigo wa zambi zetu, kusudi kwa njia yake tupate kuwa wenye haki mbele ya Mungu.