Sura 3

1 Maneno haya yanaonyesha kwamba tunaanza kujisifu tena sisi wenyewe? Au tunahitaji kuwatolea ninyi barua za ushuhuda au kuziomba kwenu kama wengine? 2 Ninyi wenyewe ni kama barua yetu ya ushuhuda iliyoandikwa katika mioyo yetu na watu wote wanaweza kuitambua na kuisoma. 3 Inaonekana wazi kwamba ninyi ni barua iliyoandikwa na Kristo na kutumwa kwa njia ya utumishi wetu. Barua hii inaandikwa si kwa wino, lakini kwa Roho wa Mungu Mwenye Uzima. Barua hiyo haikuandikwa juu ya vibao vya mawe, lakini katika mioyo ya watu. 4 Tunasema neno hili kwa ajili ya tumaini tunalokuwa nalo kwa Mungu kwa njia ya Kristo. 5 Si kusema kwamba sisi wenyewe tuko na uwezo wa kujitungia jambo hili, lakini uwezo wetu unatoka kwa Mungu. 6 Kwa maana Mungu ndiye aliyetuwezesha kuwa watumishi wa agano jipya, lisilotokana na Sheria iliyoandikwa, lakini na Roho. Sheria iliyoandikwa inaleta kifo lakini Roho analeta uzima. 7 Sheria ile inayoleta kifo imeandikwa neno kwa neno juu ya vibao vya mawe na utukufu wa Mungu ulingaa wakati ule. Uso wa Musa ukangaa vilevile hata Waisraeli hawakuweza kuangalia uso wake ingawa kungaa kule kulikuwa kwa muda tu. 8 Basi si zaidi sana matokeo ya utumishi wa Roho yatakuwa yenye utukufu? 9 Ikiwa utumishi unaowaletea watu hukumu ulikuwa na utukufu, basi si zaidi sana utumishi unaowafanya watu wahesabiwe haki mbele ya Mungu, utakuwa na utukufu mkubwa zaidi? 10 Tunaweza kusema kwamba ule utukufu uliongaa zamani hauwezi kulinganishwa na utukufu wa sasa unaokuwa mkubwa zaidi. 11 Kwa maana kama mambo yaliyokuwa ya muda tu yalipata utukufu, basi yale yanayodumu ni yenye utukufu zaidi. 12 Na kwa sababu tunakuwa na tumaini lile, sisi tunasema kwa uhodari. 13 Sisi hatufanyi kama Musa alivyokuwa akifunika uso wake na kitambaa kwa kuzuiza Waisraeli wasiangalie mwisho wa utukufu uliokuwa wa muda tu. 14 Lakini akili yao ilikuwa nzito kwa kufahamu. Kwa maana mpaka sasa, Waisraeli wanaposoma katika vitabu vya Agano la Kale, akili yao inafunikwa na kitambaa kile kile. Kitambaa kile kitaondolewa tu kwa mtu anayeungana na Kristo. 15 Mpaka sasa, kila mara wanaposoma katika vitabu vya Musa, kitambaa kinafunika mioyo yao. 16 Lakini Wakati mtu anapomurudilia Bwana, kitambaa kile kinaondolewa. 17 Hapa Bwana ni Roho; na pahali Roho wa Bwana anapokaa, pale kuna uhuru. 18 Sisi wote ambao uso haukufunikwa, tunaonyesha kama kioo utukufu wa Bwana. Kwa hiyo, tunabadilishwa kwa kufanana na Bwana, nasi tunapita toka utukufu mmoja hata utukufu mwingine unaokuwa mkubwa zaidi tena. Kwa maana kazi hii inatimizwa na Bwana ndiye Roho.