Sura 2

1 Basi, nilikusudia kutorudia tena kwenu nikiwa mwenye huzuni. 2 Kwa maana kama nikiwahuzunisha ninyi, ni nani atakayenifurahisha tena, isipokuwa tu wale niliowahuzunisha? 3 Ni kwa sababu hii niliwaandikia kwamba sitakuja tena kwenu nisihuzunishwe na watu waliopaswa kunifurahisha. Maana nina uhakika kwamba mimi ninapofurahi, ninyi wote munafurahi vilevile. 4 Niliwaandikia nikiwa mwenye kusikitika sana na mwenye kufazaika moyoni nikilia machozi mengi, si kwa kuwahuzunisha ninyi, lakini ni kusudi mupate kujua namna gani ninavyowapenda. 5 Kulikuwa mtu aliyefanya mambo ya kuhuzunisha, hakunihuzunisha mimi, lakini amewahuzunisha ninyi wote au bila kwenda mbali zaidi wamoja kati yenu. 6 Azabu mtu yule aliyopewa na watu wengi kati yenu inatosha kwake. 7 Basi sasa ni afazali kumusamehe na kumufariji, na kuepuka asikate kitumaini kwa sababu ya huzuni kubwa. 8 Kwa hiyo ninawasihi ninyi kuhakikisha upendo wenu kwa mtu yule. 9 Kwa maana shabaha yangu ya kuwaandikia ile barua ni kutaka kuwapima nipate kujua kwamba muko tayari kunitii siku zote. 10 Wakati munaposamehe mtu, nami ninamusamehe vilevile. Kwa maana kama ninasamehe, na ikiwa kweli ninakuwa na neno lolote la kusamehe, ninasamehe mbele ya Kristo kwa ajili yenu, 11 kusudi Shetani asipate njia ya kutushinda, maana tunajua nia zake. 12 Wakati nilipofika katika mji Troa kwa kutangaza Habari Njema ya Kristo, Bwana alifungua mulango wa kutumika kule. 13 Ingawa vile, nilifazaika sana kwa sababu sikumukuta ndugu yangu Tito. Halafu nikaagana na watu wa mji ule na kwenda Makedonia. 14 Lakini Mungu ashukuriwe, maana yeye ndiye anayetupatia ushindi siku zote katika ushirika wetu pamoja na Kristo. Anatutumia sisi kwa kutambulisha Kristo pahali pote kama vile harufu nzuri ya marasi inavyosambaa popote. 15 Kwa maana sisi ni kama harufu nzuri iliyotolewa na Kristo kwa Mungu; na kunukia wale wanaookolewa na wale wanaopotea. 16 Kwa wale wanaopotea ni harufu ya kifo inayoleta kifo; lakini kwa wale wanaookolewa, ni harufu ya uzima inayoleta uzima. Basi nani anayekuwa na uwezo wa kutimiza kazi ya namna hii? 17 Basi sisi si kama wengine wengi wanaochuuza neno la Mungu; lakini kwa sababu Mungu ndiye aliyetutuma, sisi tunasema ukweli mbele yake, kama vile watumishi wa Kristo.