Sura 9

1 Mimi si huru? Mimi si mutume? Mimi sikumuona Yesu Kristo Bwana wetu? Ninyi si matunda ya kazi yangu kwa ajili ya Bwana? 2 Hata ikiwa watu wengine hawakubali kuwa mimi ni mutume, ninyi munakubali kuwa mimi ni mutume. Ninyi ni kitambulisho kinachohakikisha kwamba mimi ni mutume, kwa ajili ya kuungana kwenu na Bwana. 3 Watu wanaponishitaki, mimi ninajitetea kwa namna hii: 4 basi sina haki ya kupokea chakula na kinywaji kwa ajili ya kazi yangu? 5 Au sina haki ya kusafiri pamoja na mwanamuke mukristo kama vile mitume wengine wanavyofanya, nao wandugu za Bwana na hata Petro? 6 Au ni mimi na Barnaba tu ndio tunaopaswa kujitumikia wenyewe kwa kupata vifaa vya maisha? 7 Ni askari gani anayejilipia mwenyewe vifaa vya kiaskari? Au mtu gani asiyekula matunda ya mizabibu aliyopanda? Au ni mchungaji gani asiyekunywa maziwa ya kundi analochunga? 8 Musifikiri kuwa ninasema maneno hayo kufuatana na mambo ya maisha. Hata Sheria ya Musa inasema maneno hayo vilevile. 9 Kwa maana imeandikwa hivi katika Sheria ile ya Musa: «Usifunge kinywa cha ngombe anapokanyaga nganoa.» Mungu anashugulikia ngombe? 10 Hasemi maneno haya zaidi sana kwa ajili yetu? Hakika, maneno hayo yaliandikwa kwa ajili yetu. Inafaa yule anayelima na yule anayetwanga watumike wakiwa na tumaini la kupata sehemu yao ya mavuno. 11 Ikiwa tumepanda mbegu ya kiroho ndani yenu, basi kuna jambo gani kubwa kama nasi tukitazamia kupata vifaa vya kimwili toka kwenu? 12 Ikiwa wengine wako na haki ya kupata vitu kama vile toka kwenu, sisi hatuna haki zaidi kuliko wao? Sisi hatudai kutendewa sawa na haki yetu, lakini tunavumilia kusudi tusiiwekee Habari Njema ya Kristo kizuizo chochote. 13 Munajua hakika kuwa wale wanaotumika katika hekalu wanapata chakula chao ndani ya hekalu. Na wale wanaotumika kwa kutoa sadaka juu ya mazabahu wanapata sehemu yao kutoka sadaka zile. 14 Vilevile, Bwana aliagiza kuwa wale wanaohubiri Habari Njema wanapaswa kuishi kwa njia ya Habari Njema. 15 Lakini mimi sikudai hata neno moja ya haki hizo, wala sikuandikii haya kwa kusudi la kutafuta kuzipewa. Ingekuwa heri kwangu kufa kuliko kuzuizwa na mtu yeyote kwamba nisijisifu juu ya jambo hili. 16 Mimi sina haki ya kujisifu kwa sababu ninatangaza Habari Njema, kwa maana nimelazimishwa kuitangaza. Basi ole kwangu kama nisipotangaza Habari Njema. 17 Ingekuwa nimechagua kazi hii kwa mapenzi yangu mwenyewe, ningeweza kungojea kupokea mushahara. Lakini kwa kuwa ni muzigo niliopewa, inanipasa kuitimiza. 18 Basi mushahara wangu ni gani? Mushahara wangu ni kutangaza Habari Njema bila kulipwa, maana yake bila kudai haki ninazostahili kwa kuitangaza. 19 Mimi si mutumwa wa mtu yeyote. Lakini nimejifanya kuwa mutumwa wa watu kusudi nipate wengi kati yao sawa inavyowezekana. 20 Kwa Wayuda, ninaishi kama Muyuda, kusudi niwapate Wayuda. Mimi siishi chini ya uongozi wa Sheria ya Musa, lakini kusudi niwapate wale wanaoishi chini ya Sheria ile, ninapokuwa kati yao, ninaishi kufuatana na Sheria ile. 21 Vilevile ninapokuwa kati ya wasioishi chini ya Sheria ya Musa, ninaishi kama wao, bila kuangalia Sheria, kusudi niwapate. Hii si kusema kwamba mimi sishiki sheria ya Mungu, kwa maana mimi ni chini ya uongozi wa sheria ya Kristo. 22 Na kwa wale wanaokuwa zaifu katika imani, ninajifanya kama muzaifu kusudi niwapate hao wanaokuwa zaifu. Kwa wote nimejifunza kuwa mwenye hali kama yao, kusudi nipate kuokoa wamoja kati yao kwa njia mbalimbali. 23 Ninafanya hayo yote kwa ajili ya Habari Njema kusudi nipate sehemu ya baraka zake. 24 Munajua hakika kuwa wale wanaofanya mashindano ya kukimbia, wote wanakimbia lakini ni mmoja tu anayepokea zawadi. Basi mukimbie hata mufikie kupokea zawadi. 25 Na kila mtu anayefanya mashindano katika michezo anajizuiza na vitu vingi katika mazoezi yake. Basi wanafanya hivi kusudi wapate taji yenye kuharibika; lakini sisi tunafanya vile, kusudi tupate taji isiyoharibika. 26 Ni kwa sababu hiyo ninakimbia nikiwa na shabaha ya kushinda. Mimi ni kama mupiganaji wa ngumi asiyepiga katika hewa. 27 Lakini ninatesa mwili wangu kwa mazoezi makali na kuutumikisha vikali kusudi mimi mwenyewe nisikataliwe kisha kutangaza ujumbe kwa watu wengine.