Sura 10

1 Wandugu zangu, ninataka mukumbuke kwamba babu zetu wote walisafiri wakiongozwa na wingu, nao wote walivuka katikati ya bahari Nyekundu kwa usalama. 2 Wote walibatizwa katika lile wingu na katika ile bahari kusudi wapate kuungana na Musa. 3 Wote walikula chakula kimoja cha kiroho. 4 Wote walikunywa kinywaji kimoja cha kiroho; kwa maana walikunywa maji yaliyotoka ndani ya lile jiwe lililosafiri pamoja nao, nalo jiwe lilikuwa Kristo. 5 Lakini, wengi sana kati yao hawakumupendeza Mungu, kwa hiyo wakakufia katika jangwa. 6 Mambo hayo ni mufano kwetu, kusudi tusikuwe na tamaa mbaya kama vile wao. 7 Basi musikuwe wenye kuabudu sanamu kama wamoja kati yao walivyokuwa; kama vile Maandiko haya Matakatifu yanavyosema: «Watu wakaikaa kula na kunywa na kisha wakasimama kwa kujifurahisha.» 8 Musifanye uasherati kama vile wamoja kati yao walivyofanya hata wakakufa kwa siku moja watu elfu makumi mbili na tatu. 9 Vilevile tusimupime Kristo kama vile wamoja wao walivyofanya, hata wakauawa na nyoka. 10 Musinungunike kama vile wamoja kati yao walivyofanya hata malaika mwangamizaji akawateketeza. 11 Mambo haya yote yaliwafikia kusudi yakuwe mufano kwa watu wengine; yameandikwa kwa kutuonya sisi, kwa maana tunaishi katika kipindi cha mwisho wa nyakati. 12 Kwa hiyo yule anayefikiri kwamba anasimama imara, afanye angalisho asianguke. 13 Majaribu yale munayopata, ni yale yanayowapata watu wengine wote. Mungu hatawaachilia kujaribiwa kupita nguvu zenu, kwa maana yeye ni mwaminifu. Jaribu litakapowatokea, atawapatia nguvu ya kulivumilia, hata muweze kulishinda. 14 Kwa hiyo wapenzi wangu, muepuke kutambikia sanamu. 15 Ninasema nanyi kama watu wenye akili; muamue ninyi wenyewe juu ya maneno ninayotaka kuwaambia: 16 tunapokunywa kikombe ambacho kwa ajili yake tunamutolea Mungu shukrani, basi kwa njia ya kikombe kile hatuungani na damu ya Kristo? Nasi tunapomega mukate na kuukula, kwa njia hiyo, mukate ule hautuungi na mwili wa Kristo? 17 Kwa kuwa mukate ni mmoja, ijapokuwa sisi ni wengi, tuko mwili mmoja, kwa maana sisi wote tunashiriki mukate ule mmoja. 18 Muangalie mufano wa Waisraeli: wale wanaokula vitu vinavyotolewa sadaka juu ya mazabahu wanaungana na Mungu kwa njia ya sadaka ile. 19 Basi niseme nini? Nyama iliyotambikiwa kwa sanamu ni yenye mafaa? Au kwamba sanamu ni kitu cha lazima? 20 Hapana. Ninataka kusema kwamba vitu wapagani wanavyotambikia, wanavitolea pepo wala si Mungu. Nami sipendi mushirikiane na pepo hata mara moja. 21 Hamuwezi kuchangia kikombe cha Bwana na kikombe cha pepo. Vilevile hamuwezi kuchangia meza ya Bwana na meza ya pepo. 22 Au tunataka kumuchokoza Bwana hata asikie wivu? Munafikiri kuwa sisi tuko na nguvu kuliko yeye? 23 Wamoja wenu wanasema: «Vitu vyote vinaruhusiwa. Ni kweli, lakini vyote havifai. Vitu vyote vinaruhusiwa, lakini vyote havifai kwa kujenga imani. 24 Mtu asitafute faida yake mwenyewe, lakini faida ya mwenzake. 25 Ninyi ni huru kwa kula kila kitu kinachouzishwa katika soko bila kuulizauliza neno kwa sababu ya zamiri. 26 Kwa «maana Maandiko Matakatifu yanasema: Dunia na vyote vinavyokuwa ndani yake ni vya Bwana.» 27 Kama mupagani anawaalika kula chakula, nanyi mukikubali kwenda kule, mukule vyote wanavyotoa kwenu bila kuulizauliza neno kwa sababu ya zamiri. 28 Lakini kama mtu akiwaambia ninyi: “Vyakula hivi vimetambikiwa kwa sanamu,” basi musivikule kwa ajili ya yule aliyewaarifu na kwa ajili ya zamiri. 29 Sisemi juu ya zamiri zenu, lakini juu ya zamiri ya yule aliyewaarifu. Labda kuna mtu anayeweza kuuliza: “Kwa sababu gani ninaweza kuzuizwa kutenda sawa na uhuru wangu kwa ajili ya mwingine? 30 Kama ninamushukuru Mungu kwa ajili ya chakula ninachokula, kwa nini wananiteta juu ya chakula ambacho kwa ajili yake ninamutolea Mungu shukrani?”» 31 Basi, kama mukikula au mukikunywa, au mukifanya neno lolote, mufanye yote kwa ajili ya utukufu wa Mungu. 32 Basi muangalie, kusudi musiwakwaze Wayuda, wala Wagriki, wala kanisa la Mungu. 33 Mufanye kama vile mimi: ninajikaza kwa kupendeza watu wote katika mambo yote, maana sitafuti faida yangu mimi mwenyewe, lakini faida ya watu wote, kusudi waokolewe.