Sura 11

1 Mufuate mufano wangu kama vile mimi ninavyofuata mufano wa Kristo. 2 Ninawashukuru kwa sababu munanikumbuka katika mambo yote na kwa sababu munashika mafundisho yangu sawa vile nilivyoyafundisha kwenu. 3 Lakini ninataka mufahamu maneno haya: Kristo ni kichwa cha kila mwanaume, na mwanaume ni kichwa cha muke wake, na Mungu ni kichwa cha Kristo. 4 Basi mwanaume yeyote akifunika kichwa chake wakati anapoomba Mungu, au anapotabiri, anamuzaraulisha Kristo. 5 Lakini mwanamuke yeyote asipofunika kichwa chake wakati anapoomba au anapotabiri, anamuzaraulisha mume wake. Tendo hilo linahesabiwa kama vile amenyolewa. 6 Kama mwanamuke hafuniki kichwa, anaweza basi kunyolewa! Lakini kwa sababu ni haya kwa mwanamuke kukatwa nywele au kunyolewa, basi inafaa afunike kichwa. 7 Mwanaume hapaswi kufunika kichwa, kwa sababu yeye ni mufano na utukufu wa Mungu. Lakini mwanamuke ni utukufu wa mwanaume. 8 Kwa maana mwanaume hakuumbwa kutoka katika mwanamuke, lakini mwanamuke aliumbwa kutoka katika mwanaume. 9 Na zaidi ya hii, mwanaume hakuumbwa kwa ajili ya mwanamuke, lakini mwanamuke aliumbwa kwa ajili ya mwanaume. 10 Kwa hiyo, kwa sababu ya wamalaika, mwanamuke anapaswa kufunika kichwa chake kuwa kitambulisho kinachoonyesha kuwa yuko chini ya mamlaka ya mume wake. 11 Lakini katika ushirika wetu na Bwana, hakuwezi kuwa mwanamuke pasipo mwanaume wala mwanaume pasipo mwanamuke. 12 Kwa maana kama vile mwanamuke alivyoumbwa kutoka katika mwanaume, vilevile mwanaume anazaliwa na mwanamuke; na vyote vinatoka kwa Mungu. 13 Muamue ninyi wenyewe: ni vema mwanamuke asifunike kichwa anapoomba Mungu wakati wa ibada? 14 Hali ya asili yenyewe inawaonyesha kuwa ni haya kwa mwanaume kuwa na nywele ndefu, 15 lakini ni heshima kwa mwanamuke kuwa na nywele ndefu. Kwa maana nywele ndefu zimetolewa kwa mwanamuke kwa kuwa nguo ya kufunika kichwa. 16 Lakini kama mtu akitaka kubishana juu ya neno hili, ajue kwamba sisi wala makanisa ya Mungu hatuna desturi ingine. 17 Kuelekea maonyo yanayofuata, mimi siwasifu. Kwa maana munapokusanyika, mikutano yenu haiwafalii, lakini inawaletea hasara. 18 Kwanza, ninasikia kwamba munapokusanyika kuna matengano katikati yenu, nami ninasadiki kwamba nusu ya maneno yale ni ya kweli. 19 (Inafaa kuwe matengano kati yenu, kusudi wale wanaokuwa waaminifu wa kweli kati yenu wajulikane.) 20 Munapokusanyika hamukuli karamu ya Bwana. 21 Kwa maana munapokula, kila mmoja anajiharikisha kula chakula chake mwenyewe, hivi wamoja wenu wanasikia njaa na wengine wanalewa. 22 Basi, ninyi hamuna nyumba munamoweza kukulia na kukunywea? Au munazarau kanisa la Mungu na munataka kuwapatisha haya wale wasiokuwa na kitu? Munataka niwaambie ninyi nini? Inafaa niwasifu? Hapana, siwezi kuwasifu hata kidogo juu ya jambo hilo! 23 Kwa maana haya ndiyo mafundisho niliyopokea kutoka kwa Bwana, nami niliyotoa kwenu: katika usiku ule Bwana Yesu alipotolewa, alitwaa mukate, 24 na alipokwisha kumushukuru Mungu, akaumega akisema: «Huu ni mwili wangu unaotolewa kwa ajili yenu. Mufanye hivi kwa kunikumbuka. 25 Vilevile, nyuma ya kula akatwaa kikombe na kusema: “Kikombe hiki ni agano jipya la Mungu, linalohakikishwa kwa njia ya damu yangu. Mufanye hivi kwa kunikumbuka kila mara munapokikunywa.”» 26 Kwa sababu kila mara munapokula mukate huu na kunywa kikombe hiki, munatangaza kufa kwa Bwana mpaka atakapokuja. 27 Basi kila mtu anayekula mukate wa Bwana au kunywa kikombe chake bila kustahili, anafanya zambi akikosea mwili na damu ya Bwana. 28 Basi kila mtu ajichunguze mwenyewe na kisha akule mukate huu na kunywa kikombe hiki. 29 Kwa maana mtu akikula mukate na kunywa kikombe pasipo kutambua maana ya mwili wa Bwana, anajiletea azabu yeye mwenyewe kwa kula na kunywa. 30 Na kwa sababu hii wengi kati yenu ni wagonjwa na wazaifu, na wengi wamekufa. 31 Lakini tungejichunguza sisi wenyewe kwanza, hatungehukumiwa na Mungu. 32 Lakini tunahukumiwa na kuazibiwa na Bwana kusudi tusiazibiwe pamoja na watu wa dunia hii. 33 Kwa hiyo wandugu zangu, wakati munapokusanyika kwa kula karamu ya Bwana, sherti mungojeane. 34 Kama mtu akiwa na njaa, akule katika nyumba yake, kusudi musikusanyike kwa kujiletea azabu. Basi maneno mengine yanayobaki nitayatengeneza wakati nitakapofika kwenu.