Sura 4

1 Kwa hiyo mutuhesabu kama watumishi wa Kristo, wanaoshugulika na ujumbe wa siri wa Mungu. 2 Yanayohitajika kwa mwenye madaraka kama hayo, ni kuwa mwaminifu. 3 Kwa ngambo yangu, si neno hata kidogo kuhukumiwa nanyi au na tribinali ya watu. Na hata mimi mwenyewe sijihukumu. 4 Kweli zamiri yangu hainihukumu juu ya neno lolote, lakini hii si kusema kwamba mimi ni mwenye haki. Bwana ndiye anayenihukumu. 5 Kwa hiyo musihukumu mtu mbele ya wakati uliopangwa; mungojee mpaka Bwana atakaporudia. Yeye ndiye atakayeonyesha wazi katika mwangaza mambo yote yaliyofichwa katika giza na kufunua nia za mioyo za watu. Halafu kila mtu atapokea sifa anayostahili toka kwa Mungu. 6 Wandugu zangu, nimesema maneno haya nikitwaa mufano wa Apolo na wangu mimi mwenyewe kusudi yakuwe fundisho kwenu. Nilitaka kwamba kufuatana na mufano huu mujifunze maana ya masemi haya: «Musipite pembeni ya maandiko.» Hata mtu mmoja kati yenu asijivunie mtu fulani na kuzarau mwingine. 7 Ni nani aliyekuweka kuwa mkubwa kuliko wengine? Si Mungu ndiye aliyekupa vitu vyote unavyokuwa navyo? Ikiwa ni hivi, kwa sababu gani unajivuna kama vile haukuvipewa kama zawadi? 8 Sasa mumekwisha kupata vyote munavyohitaji! Mumekwisha kuwa watajiri! Munakuwa wafalme ingawa sisi hatuko wafalme. Heri mungekuwa kweli watawala kusudi nasi vilevile tupate kutawala pamoja nanyi. 9 Kwa maana inaonekana kuwa Mungu ametufanya sisi mitume kuwa watu wenye hali ya chini kabisa. Tunahesabiwa kama watu wanaohukumiwa kufa mbele ya watu. Tumewekwa kama kitu cha kushangaza, kinachoangaliwa na dunia nzima, nao wamalaika na watu vilevile. 10 Sisi ni wapumbafu kwa ajili ya Kristo, lakini ninyi ni wenye hekima katika kuungana kwenu na Kristo. Sisi ni zaifu, lakini ninyi ni wenye nguvu. Tunazarauliwa, lakini ninyi munaheshimiwa! 11 Hata sasa, tunateswa na njaa na kiu, tunakosa nguo, tunapigwa, tunatangatanga bila makao. 12 Tunasumbuka sana tukifanya kazi kwa mikono yetu wenyewe. Wakati tunapotukanwa, tunabariki; wakati tunapoteswa, tunavumilia; 13 wakati tunaposingiziwa, tunajibu kwa upole. Hata sasa tunahesabiwa kama takataka za dunia, na kila mtu anatuangalia kama uchafu. 14 Siwaandikii maneno haya kwa kuwapatisha haya, lakini kwa kuwaonya kama watoto wangu wapendwa. 15 Hivi kuelekea maisha yenu na Kristo, hata mukiwa na walezi maelfu muko tu na baba mmoja. Kwa maana kuelekea maisha yenu na Yesu Kristo ni mimi niliyewazaa kwa njia ya kuwatangazia Habari Njema. 16 Basi ninawasihi, mufuate mufano wangu. 17 Ni kwa sababu hii ninawatumia ninyi Timoteo. Yeye ni mwana wangu mupendwa na mwaminifu mbele ya Bwana. Atawakumbusha kanuni ninazofuata katika maisha yangu na Yesu Kristo, nami ninazofundisha fasi zote katika makanisa yote. 18 Watu wamoja kati yenu wanajivuna wakifikiri kwamba sitakuja kuwaona. 19 Lakini nitakuja kwenu upesi Bwana akitaka. Basi pale nitajua maneno ya wale wanaojivuna na kujionea uwezo wao vilevile! 20 Kwa maana kazi ya Ufalme wa Mungu haionyeshwi kwa njia ya kusema tu, lakini vilevile kwa njia ya matendo ya uwezo. 21 Basi munataka nini? Nifike kule kwenu, nikikuja na fimbo au na moyo unaojaa upendo na upole?