Sura 3

1 Kweli wandugu zangu, sikuweza kusema nanyi kama watu wanaotawaliwa na Roho wa Mungu, lakini kama watu wanaotawaliwa na mambo ya kidunia. Mungali kama watoto wachanga katika mambo ya Kikristo. 2 Niliwanywesha maziwa, sikuwapa chakula kigumu, kwa maana mulikuwa hamujakiweza bado. Na hata sasa hamukiwezi, 3 kwa sababu mungali munatawaliwa na mambo ya kidunia. Kwa maana ikiwa kungali wivu na ugomvi katikati yenu, haionyeshi kwamba munatawaliwa na mambo ya kidunia, nanyi munaishi kufuatana na hali ya kimtu? 4 Wakati mmoja wenu anaposema: «Mimi ni wa Paulo na mwingine anasema: “Mimi ni wa Apolo,”» basi ninyi hamufanyi mambo ya kidunia? 5 Basi, Apolo ni nani? Na Paulo ni nani? Sisi ni watumishi wa Mungu, waliowaonyesha ninyi njia ya kuamini. Tumefanya vile kila mmoja wetu kwa kadiri ya zawadi aliyopewa na Bwana. 6 Mimi nilipanda mbegu na Apolo alinywesha maji, lakini Mungu ndiye aliyeiotesha. 7 Hivi yule anayepanda na yule anayenyweshea maji, wote si kitu; Mungu ndiye anayekuwa wa lazima kwa maana ni yeye anayeotesha mbegu. 8 Yule anayepanda na yule anayenyweshea maji wote ni sawa; naye Mungu atamupa kila mtu mushahara wake kufuatana na kazi aliyofanya. 9 Kwa maana sisi tunashirikiana na Mungu katika kazi, na ninyi ni shamba la Mungu. Vilevile ninyi ni majengo ya Mungu. 10 Kwa kadiri ya zawadi Mungu aliyonipatia, kama vile fundi wa kujenga mwenye hekima, niliweka musingi. Na sasa, mtu mwingine anajenga juu yake. Lakini inafaa kila mtu aangalie vizuri namna anavyojenga. 11 Kwa maana hakuna mtu anayeweza kuweka musingi mwingine pahali pa ule uliokwisha kuwekwa, ni kusema Yesu Kristo. 12 Mtu anaweza kujenga juu ya musingi huu na zahabu, feza, mawe ya bei kali, miti, nyasi au majani. 13 Lakini hali ya kazi ya kila mtu itaonekana wazi, kwa sababu Siku ile ya hukumu itaionyesha waziwazi. Kwa maana Siku ile itajitokeza katikati ya moto, na moto ule ndio utakaopima na kuonyesha hali ya kazi ya kila mtu. 14 Na ikiwa kile mtu alichojenga juu ya musingi huu hakiungui na moto, mtu yule atapokea zawadi. 15 Lakini kama kile alichojenga kikiungua, yeye atakosa zawadi, hata hivi yeye mwenyewe ataokolewa, lakini itakuwa kama vile ameopolewa toka ndani ya moto. 16 Hamujui hakika kuwa ninyi ni hekalu la Mungu na kuwa Roho wa Mungu anakaa ndani yenu? 17 Basi mtu akiharibu hekalu la Mungu, Mungu atamuharibu vilevile. Kwa maana hekalu la Mungu ni takatifu, na ninyi ndilo hekalu lake. 18 Mtu yeyote asijidanganye mwenyewe. Kama mtu fulani kati yenu akijizania kuwa mwenye hekima ya kidunia, ajifanye kama mupumbavu kusudi apate kuwa na hekima ya kweli. 19 Kwa maana hekima ya kidunia ni upumbavu mbele ya Mungu. Ni sawa vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: «Mungu anawanasa wenye hekima katika werevu wao wenyewe. 20 Nayo yanasema vilevile: “Bwana anatambua mawazo ya wenye hekima; anajua kwamba ni ya bure.”» 21 Basi mtu asijivune kwa ajili ya wanadamu. Kwa maana vitu vyote ni vyenu: 22 ikiwa Paulo, Apolo au Petro, dunia, uzima, kifo, mambo ya sasa au mambo yatakayokuja. 23 Lakini ninyi ni watu wa Kristo, naye Kristo ni wa Mungu.