Sura 2

1 Wandugu zangu, wakati nilipokuja kwenu kuwapasha habari ya siri ya Mungu, sikutumia maneno magumu wala hekima ya dunia. 2 Kwa maana wakati nilipokuwa pamoja nanyi nilikusudia nisijue mambo mengine lakini Yesu Kristo tu na habari ya kufa kwake juu ya musalaba. 3 Sababu ya hii nilikuwa kwenu katika hali ya uzaifu na woga, mwenye kutetemeka sana. 4 Mafundisho yangu na mahubiri yangu hayakutolewa kwa maneno ya werevu na hekima ya kimtu, lakini katika onyesho la uwezo wa Roho wa Mungu, 5 kusudi imani yenu isikuwe katika hekima ya watu, lakini katika uwezo wa Mungu. 6 Ingawa vile, mimi ninatangaza mambo ya hekima kwa watu waliokomaa kiroho. Lakini mambo haya si ya hekima ya kidunia, wala ya watawala wa dunia hii watakaoangamizwa. 7 Ninatangaza hekima ya siri ya Mungu, hekima iliyofichwa kwa watu, na iliyopangwa na Mungu mbele ya kuumbwa kwa dunia kwa ajili ya utukufu wetu. 8 Hakuna hata mutawala mmoja kati ya watawala wa dunia hii aliyeelewa hekima ile. Kama wangeielewa wasingemutundika Bwana wa utukufu juu ya musalaba. 9 Lakini ni kama vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: «Mambo yale ambayo hakuna mtu aliyepata kuyaona wala kuyasikia, mambo yale ambayo hakuna mtu aliyepata kufikiri moyoni juu yake, ndiyo yale Mungu aliyowatayarishia wale wanaomupenda.» 10 Lakini Mungu ametufunulia sisi siri yake kwa njia ya Roho wake. Maana Roho anachunguza vitu vyote, hata mipango ya Mungu inayofichwa kabisa. 11 Hakuna mtu anayeweza kujua mawazo ya mtu mwingine isipokuwa tu roho ya mtu inayokuwa ndani yake. Vilevile, hakuna anayejua mawazo ya Mungu isipokuwa Roho wa Mungu tu. 12 Na sisi hatukupokea roho ya dunia hii, lakini tulipokea Roho anayetoka kwa Mungu, kusudi tupate kujua vitu vyote tulivyojaliwa kwa neema ya Mungu. 13 Nasi tunaposema hatutumii maneno yanayotokana na hekima ya kimtu, lakini maneno yanayotokana na Roho wa Mungu, tukieleza maneno ya kiroho kwa watu wanaokuwa wa Roho. 14 Lakini mtu anayefuata hali yake ya kidunia hawezi kukubali maneno yanayotoka kwa Roho wa Mungu. Kwa sababu anayaona kuwa ni upumbavu kwake, naye hawezi kuyaelewa kwa maana yanatambulikana tu kwa njia ya Roho. 15 Mtu anayekuwa na Roho wa Mungu anahukumu mambo yote, lakini hakuna mtu anayeweza kumuhukumu. 16 Kama vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: «Ni nani anayejua mawazo ya Bwana? Ni nani anayeweza kumushauria?» Lakini sisi tuko na mawazo yanayotoka kwa Kristo.