Sura 1

1 Barua hii inatoka kwangu mimi Paulo na kwa ndugu yetu Sositeni. Ni mimi niliyeitwa na Mungu kwa mapenzi yake kuwa mutume wa Kristo Yesu. 2 Tunawaandikia ninyi kanisa la Mungu linalokuwa Korinto, ninyi ambao mumetakaswa kwa njia ya kuungana kwenu na Yesu Kristo na mumeitwa na Mungu kuwa watu wake. Vilevile barua hii ni kwa wote wanaoabudu jina la Bwana Yesu Kristo fasi zote, anayekuwa Bwana wao na Bwana wetu vilevile. 3 Tunawatakia neema na amani kutoka kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo. 4 Ninamushukuru Mungu wangu siku zote kwa ajili yenu, kwa sababu ya neema Mungu aliyowapa ninyi kwa njia ya Yesu Kristo. 5 Kwa maana katika kuungana kwenu na Kristo, mumejaliwa katika vitu vyote, zaidi sana katika mambo yanayoelekea masemi na ufahamu. 6 Ile inatokana na vile ujumbe juu ya Kristo umehakikishwa kwa nguvu kati yenu, 7 hata hamukosewi zawadi yoyote ya Mungu, mukiwa mukingojea wakati Bwana wetu Yesu Kristo atakapoonekana. 8 Ni yeye atakayewasimamisha ninyi imara mpaka mwisho kusudi musishitakiwe juu ya kosa lolote Siku ile ya kurudi kwa Bwana wetu Yesu Kristo. 9 Mungu ni mwaminifu katika ahadi zake, yeye aliyewaita ninyi muishi katika ushirika pamoja na Mwana wake Yesu Kristo, Bwana wetu. 10 Wandugu zangu, ninawasihi ninyi kwa jina la Bwana wetu Yesu Kristo, mukuwe na masikilizano kusudi matengano yasikuwe katikati yenu. Muishi katika umoja kabisa mukiwa na nia moja na wazo moja. 11 Kwa maana, wandugu zangu, nimepata habari zenu kwa njia ya jamaa ya Kloe kwamba kuko ugomvi katikati yenu. 12 Ninataka kusema: kila mmoja kati yenu anasema maneno yake mbalimbali. Mmoja anasema: «Mimi ni wa Paulo, mwingine anasema: “Mimi ni wa Apolo,” mwingine anasema: “Mimi ni wa Petro,” na mwingine anasema: “Mimi ni wa Kristo.”» 13 Munafikiri kwamba Kristo amegawanyika? Paulo ndiye aliyetundikwa juu ya musalaba kwa ajili yenu? Au mumebatizwa kwa jina la Paulo? 14 Ninamushukuru Mungu kuwa sikubatiza hata mmoja wenu isipokuwa Krispo na Gayo. 15 Hivi hakuna anayeweza kusema kwamba amebatizwa kwa jina langu. 16 Ni kweli, nilibatiza vilevile jamaa ya Stefano, zaidi ya wale sikumbuki kama nilibatiza mtu mwingine. 17 Kristo hakunituma kwa kubatiza, lakini amenituma kwa kutangaza Habari Njema. Amenituma kuitangaza bila kutumia hekima ya usemi, kusudi uwezo unaotokana na kufa kwa Kristo juu ya musalaba usihesabiwe kuwa bure. 18 Hivi, mahubiri ya kufa kwa Kristo juu ya musalaba yanahesabiwa kuwa upumbavu kwa wale wanaopotea. Lakini kwa sisi tunaookolewa ni uwezo wa Mungu. 19 Kwa maana Maandiko Matakatifu yanasema: «Nitaharibu hekima ya wenye hekima, Nitapoteza akili ya wenye akili.» 20 Basi, tuseme nini juu ya wenye hekima, walimu wa Sheria, nao wafundi wa usemi siku hizi? Mungu ameonyesha wazi kwamba hekima ya dunia hii ni upumbavu! 21 Mungu alikusudia kuwaokoa wale wanaomwamini kwa njia ya mahubiri tunayotangaza yanayoonekana kuwa mambo ya upumbavu. Amefanya vile kwa sababu, kwa njia ya hekima yao ya kimtu, watu hawakumutambua Mungu na hekima yake ya kimungu. 22 Wayuda wanaomba kuonyeshwa vitambulisho nao Wagriki wanatafuta hekima. 23 Lakini sisi tunamuhubiri Kristo aliyetundikwa juu ya musalaba, na mahubiri hayo yanahesabiwa kama kikwazo kwa Wayuda na upumbavu kwa watu wa mataifa mengine. 24 Lakini kwa wale walioitwa na Mungu, ikiwa Wayuda au Wagriki, Kristo ni kitambulisho cha uwezo na hekima ya Mungu. 25 Kwa maana mambo wanayomuhesabilia Mungu kuwa ya upumbavu, yanapita hekima ya watu; nayo mambo yale wanayomuhesabilia kuwa ya uzaifu yanapita nguvu za watu. 26 Basi wandugu zangu, mukumbuke vile mulivyoitwa na Mungu, kwamba si wengi kati yenu wenye hekima kufuatana na mafikiri ya watu; si wengi kati yenu wanaokuwa wenye nguvu, wala wenye vyeo. 27 Lakini Mungu anachagua vitu ambavyo watu wanahesabu kuwa vya upumbavu kusudi apatishe wenye hekima haya, naye amechagua vitu wanavyohesabu kuwa vya uzaifu kusudi apatishe wenye nguvu haya. 28 Mungu amechagua vitu ambavyo watu wanahesabu kuwa vya hali ya chini na vyenye kuzarauliwa, visivyokuwa na maana mbele ya macho ya watu, kusudi aharibu vile wanavyohesabu kuwa vya lazima. 29 Alifanya vile kusudi hata mtu mmoja asijivune mbele ya Mungu. 30 Lakini Mungu amewaunganisha na Yesu Kristo, naye amemufanya Kristo kuwa hekima yetu. Kwa njia ya Kristo tunahesabiwa haki mbele ya Mungu, tumekuwa watu watakatifu wa Mungu, na kukombolewa toka zambi zetu. 31 Kama vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: «Anayetaka kujivuna, ajivune kwa ajili ya Bwana.»