Sura 5

1 Habari inasikilika fasi zote kwamba kunafanyika uzinzi katikati yenu. Wanaeleza kwamba uzinzi huu ni ubaya mkubwa, usiofanyika hata katikati ya wapagani, kwa maana wanasema kwamba kuna mmoja wenu ambaye amekamata muke wa baba yake kuwa muke wake! 2 Nanyi munajaa na kiburi. Ninyi mungepaswa kuhuzunika na mtu yule aliyefanya kile kitendo, naye angepaswa kutengwa toka katikati yenu. 3 Ijapokuwa mimi ni mbali nanyi kimwili, mimi ni pamoja nanyi kiroho. Kwa hiyo nimefanya kama ningekuwa katikati yenu, maana yake, nimekwisha kumuhukumu kwa jina la Bwana wetu Yesu, yule mtu aliyetenda ubaya ule. 4 Wakati mutakapokusanyika, mimi vilevile nitakuwa pamoja nanyi kiroho, nao uwezo wa Bwana Yesu utakuwa katikati yenu. 5 Basi munapaswa kumutoa mtu yule kwa Shetani, kusudi mwili wake uharibiwe, nayo roho yake iweze kuokolewa Siku ile Bwana Yesu atakaporudi. 6 Hamuna kitu cha kujivunia! Hamujui vizuri mufano unaosema kwamba chachu kidogo inachachisha donge zima? 7 Basi mujitakase, mukiondoa ile chachu ya zamani ya zambi. Hivi mutakuwa kama donge jipya, lisilotiwa chachu, sawa vile munavyokuwa kwa kweli. Mufanye vile kwa maana Kristo amekwisha kutolewa sadaka kwa ajili yetu kama vile kondoo wa Pasaka. 8 Kwa hiyo tufanye karamu yetu ya Pasaka pasipo kutumia mikate iliyotiwa chachu; ni kusema pasipo zambi na uovu. Lakini tutumie mikate isiyotiwa chachu; ni kusema katika usafi na ukweli. 9 Katika barua niliyowatumia, niliwaandikia kwamba musishirikiane na washerati. 10 Hiyo sikusema kabisa kwamba musishirikiane na wote wanaokuwa wazinzi katika dunia hii, wala wenye tamaa, wala wanyanganyi, wala wenye kuabudu sanamu. Kwa maana kwa kujitenga nao, ingewapasa kutoka katika dunia! 11 Lakini niliwaandikia kwamba musishirikiane na mtu anayejiita ndugu mwamini, akiwa mwasherati, mwenye tamaa, mwenye kuabudu sanamu, mutukanaji, mulevi au munyanganyi. Na zaidi ya ile musichangie chakula na mtu wa namna hii. 12 Basi si kazi yangu kuhukumu wale wanaokuwa wa inje ya kanisa. Mungu ndiye atakayewahukumu. Lakini ninyi hamupaswi kuhukumu watu wa kanisa lenu? 13 Kama vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: «Mumwondoe mtu yule mubaya toka katikati yenu.»