1 Sauli alikuwa kwenye makubaliano na kifo chake. Ndipo siku hiyo yakaanza mateso makuu kinyume cha kanisa lililokuwa Yerusalemu; na waaminio wote walitawanyika katika majimbo ya Yudea na Samaria, isipokuwa mitume. 2 Watu wachamungu walimzika Stefano na kufanya maombolezo makubwa juu yake. 3 Lakini Sauli alilidhuru sana kanisa. Alikwenda nyumba kwa nyumba na kuwavuluta nje wanawake na waume, na kuwatupa gerezani. 4 Waaminio ambao walikuwa wametawanyika bado walienda wakilihubiri neno 5 Filipo akashuka katika mji wa Samaria na akamtangaza Kristo huko. 6 Baada ya makutano kusikia nakuziona ishara alizofanya Filipo; wakaweka umakini juu ya kile alichokisema. 7 Kutoka hapo watu wengi waliokuwa na pepo wachafu waliwatoka, huku wakilia kwa sauti kuu na wengi waliokuwa wamepooza na kulemaa waliponywa. 8 Na kulikuwa na furaha kubwa katika mji. 9 Lakini palikuwepo na mtu mmoja katika mji ule akiitwa Simon, ambaye hapo awali alikuwa akifanya uchawi; ambao aliutumia kuwashangaza watu wa mji wa Samaria, wakati akisema kuwa yeye ni mtu wa muhimu. 10 Wasamaria wote tangu mdogo hadi mkubwa; wakamakinika kwake huku wakisema; "mtu huyu ni ile nguvu ya Mungu ambayo ni kuu." 11 Wakamsikiliza kwa sababu alikuwa kwa uchawi wake amewashangaza kwa muda mrefu. 12 Lakini wakati walipoamini Filipo alipokuwa akitangaza juu ya ufalme wa Mungu na juu ya jina la Yesu Kristo, walibatizwa, wanaume kwa wanawake. 13 Hata Simoni mwenyewe aliamini: na baada ya kubatizwa,aliendelea kuwa na Filipo na alipoona ishara na miujiza iliyokuwa ikitendeka, alishangaa. 14 Wakati mitume wa Yerusalemu waliposikia kuwa sasa Samaria imepokea neno la Mungu, wakawatuma kwao Petro na Yohana. 15 Wakati walipokuwa washaashuka waliwaombea kwamba, wampokee Roho Mtakatifu. 16 Kwani mpaka wakati huo, Roho Mtakatifu alikuwa hajawashukia hata mmoja wao; walikuwa tu wamebatizwa kwa jina la Bwana Yesu. 17 Ndipo Petro na Yohana wakawawekea mikono, nao wakampokea Roho Mtakatifu. 18 Wakati Simoni alipoona kwamba Roho Mtakatifu ametolewa kupitia kuwekewa mikono na mitume; akataka kuwapa pesa, 19 Akasema, "Nipeni haya mamlaka, ili kila nitakayemwekea mikono apokee Roho Mtakatifu." 20 Lakini Petro akamwambia; pesa yako na iangamie pamoja nawewe, kwa sababu umefikiri kuwa karama ya Mungu inapatikana kwa pesa. 21 Hauna sehemu katika jambo hili, kwa sababu moyo wako si mnyoofu mbele za Mungu. 22 Hivyo basi, tubu uovu wako huu na kumwomba Bwana anaweza labda kukusamehe nia ya moyo wako. 23 Kwa maana naona uko katika sumu ya uchungu na kifungo cha dhambi." 24 Simoni akajibu na kusema, "Mwombeni Bwana kwa ajili yangu, kwa kuwa mambo yote mliyozungumza yasiweze kunitokea.." 25 Wakati Petro na Yohana walipokuwa wameshuhudia na kuhubiri neno la Bwana, walirudi Yerusalemu; wakihubiri injili katika vijiji vingi vya Wasamaria. 26 Basi malaika wa Bwana akanena na Filipo na kusema, "Inuka na uende kusini katika njia iendayo chini ya kutoka Yerusalemu kuelekea Gaza." ( Njia hii iko katika jangwa). 27 Akainuka na kwenda. Tazama, kulikuwa na mtu wa Ethiopia, towashi mwenye mamlaka kuu chini ya Kandasa; malkia wa Ethiopia. Ndiye aliyekuwa msimamizi wa hazina yake yote; naye alikuwa amekwenda Yerusalemu kuabudu. 28 Alikuwa akirejea ameketi garini mwake akisoma ckitabu cha nabii Isaya. 29 Roho akasema na Filipo, "Sogea karibu na gari hili ukashikamane nalo. 30 "Hivyo Filipo akamkimbilia, akamsikia akisoma katika kitabu cha nabii Isaya; akasema, Je unafahamu unachokisoma?" 31 Ndipo Muethiopia akasema, "Nitawezaje mtu asiponiongoza?" Akamsihi Filipo apande garini na kuketi pamoja naye. 32 Sasa fungu la maandiko alilokuwa akisoma Muethiopia ni hili; "Aliongozwa kama kondoo kwenda machinjioni kuchinjwa, na kama kondoo alinyamaza kimya, hakufungua kinywa chake: 33 Kwa kuhuzunishwa kwake hukumu yake iliondolewa: Nani ataeleza kizazi chake? maisha yake yameondolewa katika nchi." 34 Hivyo towashi akamwuliza Filipo, na kusema, "Nakuomba, ni nabii yupi ambaye anaongelewa habari zake, ni kuhusu yeye, au za mtu mwingine"?. 35 Filipo alianza kuzungumza, na kuanzia andiko hili la Isaya alimtangazia injili kuhusu Yesu. 36 Wakiwa njiani, wakafika mahali penye maji,' towashi akasema, "Tazama, pana maji hapa. Nini kinazuia nisibatizwe?, 37 "Filipo akamwambia, "Ukiamini kwa moyo wako wote unaweza kubatizwa". Hivyo Muethiopia akajibu "Naamini kwamba Yesu Kristo ni Mwana wa Mungu,". 38 Ndipo Muethiopia akaamuru gari lisimame. Walikwenda ndani ya maji, Filipo pamoja na towashi, na Filipo akambatiza. 39 Wakati walipotoka kwenye maji, Roho wa Bwana akamnyakua Filipo mbali; towashi hakumwona tena, akaenda njia yake akifurahia. 40 Lakini Filipo akatokea Azoto. Alipita katika mkoa ule na kuhubiri injili katika miji yote mpaka alipofika Kaisaria.