Sura 14

1 Mujikaze mukuwe na upendo. Vilevile mutamani sana kupata zawadi za Roho, hasa zaidi zawadi ya kutabiri. 2 Mtu anayesema kwa luga ya ajabu hasemi na watu lakini anasema na Mungu, kwa maana hakuna mtu anayemusikia. Kwa uwezo wa Roho, mtu yule anasema mafumbo. 3 Lakini yule anayetabiri anasema na watu maneno ya kuwajenga katika imani, kuwatia moyo na kuwatuliza. 4 Yule anayesema kwa luga ya ajabu anajenga imani yake mwenyewe, lakini yule anayetabiri anajenga imani ya kanisa zima. 5 Ninataka ninyi wote museme kwa luga za ajabu, lakini ninataka zaidi tena mupate kutabiri. Kwa maana, yule anayetabiri ni wa lazima kuliko yule anayesema kwa luga za ajabu, isipokuwa kama huyo mtu anaweza kutafsiri yale anayosema kusudi kanisa zima lijengwe katika imani. 6 Basi wandugu zangu, nitawafalia nini kama nikikuja kwenu na kusema nanyi katika luga za ajabu? Sitawafalia kitu pasipo kuwaelezea maneno ya ufunuo, au ya elimu, pasipo kuwatabiria au kuwafundisha. 7 Tuangalie mufano wa vyombo vya muziki kama vile filimbi au kinanda. Milio ya vyombo hivi isipokuwa mbalimbali, namna gani mtu anavyoweza kutambua wimbo unaopigwa? 8 Ngunga isipopigwa kwa mulio wa kuarifu, askari gani atakayeweza kujitayarisha kwa vita? 9 Ni hivi vilevile mambo munayosema yatatambulikana namna gani ikiwa maneno munayoeleza kwa luga za ajabu hayako wazi? Kwa maana mutakuwa kama wenye kusema na upepo. 10 Kuna namna mbalimbali za luga katika dunia, lakini hakuna hata moja isiyokuwa na maana. 11 Basi kama nisipojua luga fulani, nitakuwa kama mujinga kwa yule anayeisema, naye atakuwa kama mujinga kwangu. 12 Hivi vilevile kufuatana na vile munavyotamani sana zawadi za Roho, mujikaze kupata kwa uwingi zile zinazoweza kujenga kanisa katika imani. 13 Kwa hiyo yule anayesema kwa luga ya ajabu, aombe Mungu amupatie uwezo wa kuitafsiri. 14 Kwa maana kama nikiomba katika luga ya ajabu, roho yangu inaomba, lakini akili yangu haitumiki. 15 Basi ninapaswa kufanya nini? Nitaomba katika roho na katika akili vilevile. Nitaimba katika roho na katika akili vilevile. 16 Kwa maana kama ukimwomba Mungu ndani ya roho tu kwa kumushukuru, mtu asiyeelewa kitu anayehuzuria katika mkutano hawezi kusema amina kwa kuitikia maombi yako ya kushukuru. Ni kwa sababu hasikii mambo unayosema. 17 Ijapokuwa ni kweli maombi yako ya kushukuru yanawezekana kuwa mazuri, lakini hayajengi mtu mwingine katika imani. 18 Ndiyo, ninamushukuru Mungu kwamba ninasema kwa luga za ajabu kuliko ninyi wote. 19 Lakini, katika mkutano ninapenda kusema maneno matano yenye kusikilika, kusudi niwafundishe wengine, kuliko kusema maneno elfu kumi kwa luga za ajabu. 20 Wandugu zangu, musikuwe kama watoto kwa kufikiri: lakini katika mambo mabaya, iwatokee kutenda kama watoto wachanga. Inafaa mafikiri yenu yakuwe kama ya watu wazima. 21 Imeandikwa katika Sheria: «Bwana anasema: “Nitasema na watu hawa kwa njia ya wageni wenye luga ngeni Na hata hivi hawatanisikiliza.”» 22 Kwa hiyo, zawadi ya kusema luga za ajabu ni kitambulisho kwa wasioamini, lakini si kwa waamini. Na zawadi ya kutabiri ni kitambulisho kwa waamini, lakini si kwa wasioamini. 23 Basi kama kanisa zima limekusanyika, na watu wote wanaanza kusema kwa luga za ajabu; na kisha watu wasioelewa kitu au wasioamini wakiingia katika mkutano wenu hawatasema kuwa ninyi ni wenda-wazimu? 24 Lakini kama wote wakitabiri, na kama mtu mmoja asiyeamini au asiyeelewa kitu anaingia, atapata uhakikisho kutokana na maneno ya hao wote. Naye atahukumiwa kufuatana na yote aliyosikia na 25 kufichuliwa waziwazi mawazo yake aliyoficha. Na hivi atainama uso mpaka chini na kumwabudu Mungu, akisema: «Kweli Mungu ni katikati yenu!» 26 Wandugu zangu, niseme nini basi? Wakati munapokusanyika kwa ibada, mmoja anaweza kuimba wimbo, mwingine kufundisha, mwingine kutoa ufunuo, mwingine kusema kwa luga za ajabu na mwingine anaweza kutafsiri. Na hayo yote yanapaswa kufanyika katika nia ya kujenga kanisa katika imani. 27 Kukiwa wenye kusema kwa luga za ajabu, inafaa wasikuwe zaidi ya wawili au watatu, nao waseme mmoja kwa mmoja. Na tena kunapaswa kuwa mtu wa kutafsiri maneno wanayosema. 28 Kama hakuna mtu anayetafsiri, basi kila mmoja wao anyamaze katika mkutano, aseme tu ndani ya moyo, yeye mwenyewe na Mungu. 29 Na kwa upande wa wale wanaotabiri, wanaweza kusema wawili au watatu na watu wengine wapime yale wanayosema. 30 Lakini kukiwa mtu anayesema, na mwingine anayekaa karibu akipata ufunuo, inafaa yule anayesema anyamaze. 31 Kwa maana ninyi wote munaweza kutabiri mmoja kwa mmoja, kusudi wote wapate kufundishwa na kutiwa moyo. 32 Moyo ya unabii inapaswa kuwa chini ya utawala wa yule aliyeipewa, 33 kwa maana Mungu hataki sisi tuishi katika fujo, lakini katika amani. Sawa vile inavyokuwa desturi katika makanisa yote ya watu wa Mungu, 34 wanawake wanapaswa kukaa kimya katika mikutano ya kanisa. Wao hawaruhusiwi kusema katika kanisa, lakini wanapaswa kutii sawa vile Sheria inavyosema. 35 Kama wakiwa na neno la kuuliza, waulize waume wao kwenye nyumba zao. Ni haya kwa mwanamuke kusema katika mkutano wa kanisa. 36 Munazani kwamba Neno la Mungu limetoka kwenu au limewafikia ninyi peke yenu tu? 37 Kama mtu akizani kwamba yuko na zawadi ya unabii au zawadi ingine ya Roho, anapaswa kujua kwamba maneno haya ninayowaandikia ninyi ni amri ya Bwana. 38 Lakini kama yeye hajui vile, basi mtu asishugulike naye. 39 Kwa hiyo wandugu zangu, mutamani sana kupata zawadi ya kutabiri, nanyi musiwazuize watu kusema kwa luga za ajabu. 40 Lakini maneno yote yatendeke katika usawa na katika utaratibu.