1 Paulo akawakazia macho wale washauri wa Baraza Kubwa na kusema: «Wandugu zangu, mpaka leo zamiri yangu hainihukumu juu ya kitu chochote kinachoelekea mwenendo wangu mbele ya Mungu. 2 Paulo aliposema maneno hayo, Kuhani Mkubwa Anania akawaamuru wale waliosimama karibu naye wamupige kofi kwenye kinywa. 3 Halafu Paulo akamwambia: “Mungu yeye mwenyewe atakupiga kofi, wewe unayeonekana kwa inje kama ukuta uliopakaliwa chokaa! Wewe unaikaa pale kwa kunihukumu kufuatana na Sheria. Lakini wewe mwenyewe unaivunja kwa kuamuru wanipige!” 4 Watu waliokuwa wakisimama karibu na Paulo wakamwambia: “Wewe unamutukana Kuhani Mkubwa wa Mungu!” 5 Paulo akasema: “Wandugu zangu, sikujua kwamba yeye ni Kuhani Mkubwa. Kwa maana imeandikwa katika Maandiko Matakatifu: Usimulaani mkubwa wa taifa lako.” 6 Halafu Paulo alikuwa akijua kwamba watu wamoja katika Baraza Kubwa walikuwa Wasadukayo na wengine Wafarisayo. Kwa hiyo akasema kwa sauti katika baraza: “Wandugu zangu, mimi ni Mufarisayo, mwana wa Mufarisayo. Mimi ninahukumiwa kwa sababu ninatumaini kwamba wafu watafufuka.” 7 Alipokwisha kusema maneno hayo, kukatokea ugomvi kati ya Wafarisayo na Wasadukayo, nao mkutano ukagawanyika. 8 (Ilitokea vile kwa maana Wasadukayo wanasema kwamba wafu hawatafufuka na kwamba hakuna wamalaika, wala roho; lakini Wafarisayo wanakubali mambo hayo yote.) 9 Basi kukakuwa makelele mengi, na walimu wamoja wa Sheria waliokuwa wa chama cha Wafarisayo wakasimama na kubishana kwa nguvu, wakisema: “Hatuoni ubaya wowote juu ya mtu huyu. Labda roho au malaika wamesema naye!” 10 Ugomvi ulipozidi sana, jemadari akaogopa kwamba watu wale watamurarua Paulo. Kwa hiyo akaamuru waaskari waende katikati ya mkutano ule na kumwondosha Paulo kwa kinguvu katikati yao na kumurudisha ndani ya upango wa waaskari. 11 Usiku ule ule Bwana akamutokea Paulo, akamwambia: “Ujipe moyo! Sawa vile ulivyotoa ushuhuda juu yangu hapa Yerusalema, ni vile vile utakavyopaswa kuutoa katika Roma.”» 12 Kesho yake kulipokucha, Wayuda wakafanya shauri; wakafanya kiapo kwamba hawatakula wala kunywa mpaka wamuue Paulo kwanza. 13 Na wale waliofanya shauri lile walikuwa zaidi ya watu makumi ine. 14 Wakaenda kuwaona Makuhani Wakubwa na wasimamizi wa watu na kuwaambia: «Sisi tumefanya kiapo; hatutasubutu kula kitu chochote mpaka tumuue Paulo kwanza. 15 Basi sasa, ninyi pamoja na Baraza Kubwa mumwombe jemadari awaletee Paulo, mukimwambia tu kwamba munataka kuchunguza vizuri zaidi maneno yake. Na sisi tuko tayari kumwua mbele hajafika hapa. 16 Lakini mupwa wa Paulo akapata habari ya vile watu wale wanavyovizia kumwua Paulo. Halafu akaenda katika upango wa waaskari na kumujulisha Paulo habari ile. 17 Basi Paulo akaita mmoja wa wakubwa wa waaskari na kumwambia: “Umupeleke kijana huyu kwa jemadari kwa maana yuko na neno la kumwambia.” 18 Yule mkubwa akaenda pamoja naye kwa jemadari na kumwambia: “Yule mufungwa Paulo aliniita, akaniomba nikuletee kijana huyu kwa sababu yuko na neno la kukuambia.” 19 Jemadari akamushika yule kijana mukono akaenda naye pembeni na kumwuliza: “Uko na habari gani ya kuniambia?” 20 Kijana akasema: «Wayuda wamepatana kukuomba umulete Paulo kesho katika Baraza Kubwa. Nao watakuambia tu kwamba wakubwa wa baraza wanataka kuchunguza vizuri zaidi maneno yake. 21 Lakini wewe usikubali ombi lao, kwa sababu kuna watu zaidi ya makumi ine wanaovizia kumwua. Watu hawa wamefanya kiapo kwamba hawatakula wala kunywa mpaka wamuue Paulo kwanza.» 22 Yule jemadari akamwagiza yule kijana kwamba asimwambie mtu yeyote kwamba amemupasha habari hiyo, kisha akaagana naye. 23 Kisha jemadari akawaita wakubwa wawili wa waaskari wake, akawaambia: «Mutayarishe waaskari mia mbili, waaskari wapanda-farasi makumi saba, na waaskari wapiga mikuki mia mbili kwa kwenda Kaisaria saa tatu ya usiku. 24 Mutayarishe vilevile farasi wa kumubeba Paulo kusudi afike salama kwa liwali Feliki. 25 Naye akaandika barua hii: 26 “Mimi Klaudio Lusia, ninakuandikia wewe muheshimiwa Liwali Feliki, pokea salamu zangu. 27 Wayuda walikuwa wamemukamata mtu huyu na kutaka kumwua. Nami nilipopata habari kwamba yeye ni mwanainchi wa Roma, nikaenda na kundi la waaskari na kumwokoa. 28 Na kwa kuwa nilitaka kujua sababu gani Wayuda walimushitaki, nikamufikisha mbele ya Baraza yao Kubwa. 29 Nikatambua kwamba wamemushitaki juu ya ubishi wenye kuelekea Sheria yao, lakini hakutenda kosa lolote linalomupasa kuuawa wala kufungwa. 30 Na wakati nilipopata habari kwamba Wayuda wanafanya shauri la kumwua, mara moja nikakusudia kumutuma kwako, nami nimewaagiza watu wanaomushitaki walete mashitaki yao kwako.” 31 Basi wale waaskari wakafanya kama vile walivyoamuriwa. Wakamutwaa Paulo, na usiku ule ule wakamufikisha mpaka Antipatiri. 32 Kesho yake waaskari waliotembea kwa miguu wakarudi Yerusalema kwenye upango wa waaskari. Wakawaacha waaskari wapanda-farasi waendelee pamoja na Paulo. 33 Nao walipofika Kaisaria, wakamupa liwali ile barua na kumuleta Paulo kwake. 34 Liwali akasoma barua ile na kumwuliza Paulo: “Wewe ni mtu wa jimbo gani?” Aliposikia kwamba yeye ni mtu wa jimbo la Kilikia, 35 akamwambia: «Nitakusambisha wakati wale wanaokushitaki watakapofika.» Kisha akaamuru Paulo alindwe katika nyumba ya kifalme ya Herode.