1 Nyuma ya mambo hayo, Paulo akatoka Atene, na kwenda katika mji wa Korinto. 2 Kule akakutana na Muyuda aliyeitwa Akila, muzaliwa wa jimbo la Ponto, na jina la muke wake lilikuwa Prisila. Katika siku zile walikuwa wangali wakitoka katika inchi ya Italia, kwa sababu mutawala Klaudio alikuwa ameamuru kwamba Wayuda wote watoke Roma. Paulo akaenda kuwatembelea kwao. 3 Naye akakaa na kutumika pamoja nao, kwa maana wote walikuwa wafundi wa kutengeneza hema. 4 Na kila siku ya Sabato, Paulo alibishana na Wayuda na Wagriki katika nyumba ya kuabudia na kuwashinda. 5 Sila na Timoteo walipofika toka Makedonia, Paulo akajitolea sana kwa kuhubiri Neno la Mungu, akihakikisha kwa Wayuda kwamba Yesu ndiye Kristo. 6 Lakini wakati Wayuda walipingana naye na kumutukana, kwa hiyo akakunguta mavumbi yaliyorukia juu ya nguo zake na kuwaambia: «Lazima ya kuazibiwa kwenu ikuwe juu ya kichwa chenu wenyewe! Mimi sina kosa. Tangu sasa nitawaendea watu wa mataifa mengine. 7 Halafu Paulo akaondoka pale, akaenda kukaa katika nyumba ya mtu mmoja aliyeitwa Tito Yusto, aliyekuwa mwenye kuogopa Mungu. Nyumba ya mtu huyu ilikuwa karibu sana na nyumba ya kuabudia. 8 Na Krispo, mkubwa wa nyumba ya kuabudia, akamwamini Bwana pamoja na watu wote wa nyumba yake. Nao Wakorinto wengi waliomusikiliza Paulo wakaamini na kubatizwa. 9 Siku moja usiku, Bwana akamwambia Paulo katika maono: “Usiogope, uendelee tu kusema, wala usinyamaze, 10 kwa maana mimi ni pamoja nawe. Hakuna mtu katika mji huu atakayesubutu kukukamata kwa kukutendea vibaya, kwa maana ndani yake kutakuwa watu wengi watakaonigeukia.” 11 Na Paulo akakaa kule kwa muda wa mwaka mmoja na miezi sita, akiwafundisha watu Neno la Mungu. 12 Katika nyakati Galio alipokuwa liwali wa jimbo la Akaya, Wayuda wakamufanyia Paulo shauri baya kwa nia moja, wakamukamata na kumupeleka mbele ya tribinali, 13 na kumushitaki: “Mtu huyu anawavuta watu kumwabudu Mungu kwa njia isiyopatana na Sheria yetu.” 14 Paulo alipotaka kusema, Galio akawaambia Wayuda: “Kama mungemushitaki mtu huyu juu ya neno la uovu au kosa kubwa alilofanya, ningewasikiliza ninyi Wayuda vema. 15 Lakini kwa kuona ni mabishano tu juu ya maneno, majina na sheria yenu, maneno yale yanawaangalia ninyi wenyewe. Mimi sitakata maneno yale.”» 16 Na kisha akawafukuza toka ndani ya tribinali. 17 Basi wakamukamata Sositeni, mkubwa wa nyumba ya kuabudia, wakamupiga pale mbele ya tribinali. Lakini Galio hakushugulika na jambo hilo. 18 Paulo akaendelea kule Korinto kwa muda wa siku nyingi. Kisha akaagana na wandugu waamini, akasafiri kwa njia ya chombo na kwenda katika inchi ya Suria. Nao Prisila na Akila walikuwa pamoja naye. Mbele ya kuondoka, Paulo alinyolewa kwenye kivuko cha Kenkurea, kwa maana alikuwa ametimiza kiapoa alichofanya mbele ya Mungu. 19 Walipofika Efeso, Paulo akawaacha wale wenzake kule. Naye mwenyewe akaingia ndani ya nyumba ya kuabudia na kubishana na Wayuda. 20 Nao wakamusihi akae nao muda murefu zaidi, lakini hakukubali. 21 Alipoagana nao, akawaambia: «Kama Mungu akitaka nitarudi huku kwenu tena.» Halafu akaondoka Efeso, akisafiri kwa njia ya chombo. 22 Naye alipofika katika mji Kaisaria, akaenda Yerusalema kwa kusalimia kanisa. Kisha akaenda Antiokia. 23 Alipokwisha kukaa Antiokia kwa siku chache, akaondoka kule, akapita mji kwa mji toka katika inchi ya Galatia mpaka katika inchi ya Furigia, na kule akawatia wanafunzi nguvu. 24 Katika siku zile, Muyuda mmoja, jina lake Apolo, mzaliwa wa mji Alesandria, alikuwa amefika katika mji Efeso. Alikuwa mtu mwenye uwezo katika masemi na mwenye kuelewa sana Maandiko. 25 Mtu huyu alikuwa amefundishwa Njia ya Bwana, naye alitangaza kwa bidii sana na kufundisha kwa ukweli habari za Yesu. Lakini alikuwa akijua tu ubatizo wa Yoane. 26 Yeye akaanza kusema pasipo woga katika nyumba ya kuabudia. Prisila na Akila walipomusikia, wakaenda naye kwao na kumufasiria Njia ya Mungu kwa ukweli zaidi. 27 Apolo alipotaka kwenda katika jimbo la Akaya, wandugu waamini wakamutia moyo, nao wakawaandikia wanafunzi wa kule kwamba wamukaribishe vizuri. Na wakati alipofika kule, akawasaidia sana wale walioamini kwa nguvu ya neema ya Mungu, 28 kwa maana alibishana na Wayuda mbele ya watu wote na kuwashinda kabisa. Aliwaonyesha kwa njia ya Maandiko Matakatifu kwamba Yesu ndiye Kristo